MASOMO YA MISA JUMATATU , MACHI 16, 2026

MASOMO YA MISA JUMATATU , MACHI 16, 2026

Mar 16, 2026


🟣 Juma la 4 la Kwaresima


🟣 Somo I

Isa. 65:17-21
 
Bwana asema: Tazama, mimi naumba mbingu mpya na nchi mpya, na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo; maana, tazama, naumba Yerusalemu uwe shangwe, na watu wake wawe furaha.
 
Nami nitaufurahia Yerusalemu, nitawaonea shangwe watu wangu; sauti ya kulia haitasikiwa ndani yake tena, wala sauti ya kuomboleza. Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa. Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake.
 
Neno la Bwana… Tumshukuru Mungu.

🟣 Wimbo wa Katikati


Zaburi 30:1, 3–5, 10–12
(K) Nitakutukuza, ee Bwana, kwa maana umeniinua.

Ee Bwana, nitakutukuza kwa maana umeniinua,
wala hukuwafurahisha adui zangu juu yangu.
Umeniinua nafsi yangu, ee Bwana, kutoka kuzimu;
umenihuisha na kunitoa miongoni mwao washukao shimoni. (K)

Mwimbieni Bwana zaburi, enyi watauwa wake,
mkamshukuru kwa kumbukumbu la utakatifu wake.
Maana ghadhabu zake ni za kitambo kidogo,
katika radhi yake mna uhai.
Huenda kilio huja kukaa usiku,
lakini asubuhi huwa furaha. (K)

Ee Bwana, usikie, unirehemu;
Bwana, uwe msaidizi wangu.
Uligeuza matanga yangu kuwa machezo;
ulinivua gunia, ukanivika furaha.
Ee Bwana, Mungu wangu,
nitakushukuru milele. (K)


🟣 Shangilio la Injili


(Eze. 33:11)

Bwana asema:
Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu,
bali aiache njia yake mbaya, akaishi.


🟣 Injili 


 

Yn. 4:43-54

Baada ya siku mbili hizo Yesu aliondoka huko, akaenda Galilaya. Kwa maana Yesu mwenyewe alishuhudia ya kwamba nabii hapati heshima katika nchi yake mwenyewe. Basi alipofika Galilaya, Wagalilaya walimpokea; kwa kuwa wameyaona mambo yote aliyoyatenda huko Yerusalemu wakati wa sikukuu; maana hao nao waliiendea sikukuu.

Basi alifika tena Kana ya Galilaya, hapo alipoyafanya yale maji kuwa divai. Na palikuwa na diwani mmoja ambaye mwanawe hawezi huko Kapernaumu. Huyo aliposikia ya kwamba Yesu amekuja kutoka Uyahudi mpaka Galilaya, alimwendea, akamsihi ashuke na kumponya mwanawe; kwa maana alikuwa kufani. Basi Yesu akamwambia, Msipoona ishara na maajabu hamtaamini kabisa? Yule diwani akamwambia, Bwana, ushuke asijakufa mtoto wangu. Yesu akamwambia, Enenda; mwanao yu hai. Mtu yule akalisadiki lile neno aliloambiwa na Yesu, naye akashika njia. Hata alipokuwa akishuka, watumwa wake walimlaki, wakisema ya kwamba mtoto wake yu hai. Basi akawauliza habari ya saa alipoanza kuwa hajambo; nao wakamwambia, jana, saa saba, homa ilimwacha. Basi babaye akafahamu ya kuwa ni saa ile ile alipoambiwa na Yesu, Mwanao yu hai. Akaamini yeye na wote wa nyumbani mwake.
Hiyo ni ishara ya pili aliyoifanya Yesu, alipokuwa ametoka Uyahudi kufika Galilaya.

Neno la Bwana… Sifa kwako Ee Kristo.

Wasiliana Nasi

Dar es Salaam, Tanzania

+255 758 096 383

[email protected]

Tufuatilie

© Mkatoliki Kiganjani. Haki Zote Zimehifadhiwa.